Gavana wa zamani wa Massachusetts Mitty Romney ameshinda katika uchaguzi wa awali  uliofanyika kwenye jimbo la New Hampshire wa kumpata mgombea kiti cha rais kwa tiketi ya chama cha Repuplican. Ushindi huo ni hatua kubwa ya kusonga mbele kupata uteuzi wa  chama chake kukabiliana na Rais Barack Obama katika uchaguzi mkuu wa mwezi Novemba.

Takribani kura zote zikiwa zimehesabiwa, Romney alishinda kwenye jimbo hilo kwa asilimia 39, ambapo nafasi ya pili ilichukuliwa na mbunge wa Texas, Ron Paul aliyepata asilimia 23. Balozi wa zamani wa Marekani nchini China, Jon Huntsman alishika nafasi ya tatu akiwa na asilimia 17 ya kura.

Romney aliwaambia wafuasi wake katika jimbo hilo “limeweka historia”. Ni mrepublican  wa kwanza kushinda mfululizo chaguzi mbili za awali huko  Iowa na New Hampshire katika kinyang’anyiro kikali  kwa zaidi ya miaka 30.

Romney pia alimkosoa Rais Barack Obama, akimuita “Rais aliyeshindwa”. Alikosoa masuala mbali mbali kuhusu sera za Bwana Obama na kusema ataipeleka nchi katika njia tofauti.

Wachambuzi wengi wa masuala ya kisiasa walitabiri Romney atashinda New Hampshire. Lakini mapambano katika nafasi ya pili na ya tatu  pia ni muhimu, ambapo itasaidia kutambua wagombea gani wanaendelea kuwepo katika kinyang’anyiro hicho.