blank

About VOA | Contact VOA News

Makala Maalum - Siasa Habari mpya 6:10 UTC Jumatano 20 Oktoba 2010

Uchaguzi Tanzania 2010

Jakaya Mrisho Kikwete: Awania awamu ya pili

Na Sunday Shomari

Jakaya Mrisho Kikwete

Rais Jakaya Mrisho Kikwete anawania awamu ya pili ya uongozi kama rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania baada ya kushinda katika uchaguzi wa mwaka 2005. Alianza kampeni yake mwaka huu akiwa mbele kabisa ya wapinzani wake kutokana na umaarufu wake kama kiongozi aliye madarakani, na pia mwanasiasa mwenye uzoefu wa siku nyingi.

Rais Kikwete ni mwanasiasa aliyekuwa katika siasa za chama tawala Tanzania, tangu enzi za TANU ambako kazi yake ya kwanza katika chama hicho ilikuwa kama katibu msaidizi wa TANU wa mkoa wa Singida, nafasi iliyompa nafasi ya kufanya kazi katika ngazi ya awali kabisa katika maeneo ya vijijini na wilaya za Tanzania.

Rais Kikwete pia alinoa mbinu zake za uongozi kwenye jeshi, ambako alifikia cheo cha Luteni Kanali mpaka alipojiuzulu mwaka 1992, akachagua kuwa mwanasiasa. Mwaka 1982 alichaguliwa kuingia kwenye halmashauri kuu ya CCM, na mwaka 1997 alichaguliwa kuingia katika kamati kuu ya chama hicho.

Aliingia bungeni kwa mara ya kwanza 1978 na baada ya hapo aliteuliwa kuongoza wizara mbali mbali katika serikali ya Tanzania. Mwaka 1994 akiwa na umri wa miaka 44, alikuwa ni mmoja wa mawaziri vijana kushika wizara nyeti ya fedha. Desemba 1995 aliteuliwa kuwa waziri wa mambo ya nje na alishika wadhifa huo kwa miaka 10, hadi alipochaguliwa kama rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania katika uchaguzi wa mwaka 2005.

 

Dr. Mutamwega Mugahywa

Na Mary Mgawe

Wasifu wa Dk. Mugahywa

Ukiwauliza wengi wanaomfahamu Dr. Mutamwega Mugahywa, mgombea wa chama cha Tanzania Labor Party, watakwambia kwa tabia ni mkimya na anaonekana mwenye busara katika kufanya maamuzi yake. Ni mzaliwa wa kijiji cha Igundu, Mwibara wilaya ya Kunda mkoani Mara Tanzania. Ana umri wa miaka 42.

Alipata elimu ya msingi mkoani mara na elimu ya sekondari katika shule ya Mugeza huko Bukoba na kumaliza kitado cha sita katika shule ya Tambaza jijini Dar es Salaam. Alijiunga katika chuo cha ufundi cha Mbeya na kupata mafunzo mengine nje ya nchi kama vile Zimbabwe, India na Uingereza ambako alipata shahada ya juu ya udaktari katika biashara.

Dr. Mugahywa , alianza kupata ndoto ya kisiasa kuanzia mwaka 1990 akiwa kijana mdogo kabisa aliyependa mageuzi ndani ya taifa la Tanzania, hali iliyompeleka kuanza kujipenyeza kwenye jukwaa la kisiasa na kuwa miongoni mwa kundi la vijana waliochochea mageuzi mwaka 1992 katika jiji la Dar es Salaam.

Pamoja na ukimya wake mwaka 1995 aligombea ubunge katika jimbo la Mwibara kupitia tiketi ya TLP, na kunyakua jimbo hilo alilowakilisha mpaka mwaka 2000, katika uchaguzi mwingine ambapo alichaguliwa tena na kukaa katika uwakilishi huo kwa miaka mingine mitano.

Katika uchaguzi wa mwaka 2005 alishindwa katika uchaguzi wa Mwibara kupitia chama hicho hicho cha TLP, na kupoteza uwakilishi wake katika bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kwa kutumia uzoefu wake wa ubunge wa miaka kumi na kuwepo ndani ya jukwaa la siasa kwa miaka 20 ndoto yake haikuishia kwenye kushindwa ubunge, bali kuendelea mbele na kutafuta kuwa rais ndani ya upinzani wa TLP. Katika kampeni zake amesema Moja ya kipaumbele chake mara atakapochaguliwa kuwa rais wa Tanzania Oktoba 31 ni kutoa elimu bure.

 

Peter Kuga Mziray: Mgombea urais chipukizi

Na Mkamiti Kibayasi

Peter Kuga Mziray, ni mgombea urais kwa mara ya kwanza kupitia chama cha African Progressive Party of Tanzania, ATTP-Maendeleo. Alianza kujihusisha na masuala ya siasa mwaka 1995 baada ya kujiunga na chama cha upinzani cha NCCR-Mageuzi, na kuwania ubunge wa jimbo la Same Mashariki, mkoani Kilimanjaro lakini hakufanikiwa.

Baadaye Bwana Mziray alihamia chama cha Tanzania Labour party-TLP na kushiriki katika kinyang’anyiro cha kiti hicho hicho cha ubunge huko Same Mashariki na tena hakufanikiwa, huku ushindi ukienda aliyekuwa waziri wa fedha Daniel Yona katika uchaguzi wa mwaka 2000.

Mwaka 2001 Mziray alikuwa mmoja kati ya wagombea waliowania kiti cha bunge la Afrika Mashariki, kiti ambacho kilichukuliwa na Mabere Marando.

Mziray hakuishia hapo kwani katika uchaguzi wa mwaka 2005 alijaribu tena kuwania ubunge kwa mara ya tatu huko Same Mashariki na kushindwa, wakati huu na Anna Kilango Malecela.

Chama cha ATTP-Maendeleo kilijisajili kama chama cha kisiasa mnamo mwezi Disemba mwaka 2001 na kuwasilisha wagombea wake wa majimbo kadhaa nchini Tanzania kupitia chama hicho katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005.

Mziray alizaliwa Same, Kiurio katika mkoa wa Kilimanjaro miaka 51 iliyopita. Alipata elimu ya msingi katika shule ya Kiurio huko Moshi, na alijiunga na elimu ya sekondari katika shule ya Pugu, Dar-Es-Salaam mwaka 1973 na aliendelea na kidato cha tano na sita katika sekondari ya Mkwawa mwaka 1977.

Mziray alijiendeleza na masomo ya juu ambapo mwaka 1983-1989 alihudhuria Chuo Kikuu cha Lumumba, Russia na kupata shahada ya mifugo na uchumi wa kilimo. Pia alipata shahada ya kilimo na uchumi katika chuo kikuu cha Reading huko Uingereza, mwaka 1992.

Amewahi kufanya kazi katika benki ya NBC na katika wizara ya kilimo nchini Tanzania, kabla ya kujihusisha na masuala ya siasa. Mbali na hayo alikuwa mshauri wa masuala ya mifugo katika taasisi ya kitaifa ya kupandikiza mbegu za mifugo mkoani Arusha tangu mwaka 1992.

 

Maalim Seif Shariff Hamad: Mgombea asiyehitaji utambulisho

Na Aida Issa

Maalim Seif Shariff Hamad

Wasifu wa Maalim Seif Shariff

Maalim Seif Shariff Hamad ni mgombea urais kisiwani Zanzibar ambaye haitaji utambulisho nchini Tanzania. Anawania nafasi hiyo kupitia tiketi ya chama cha Civic United Front – CUF – kwa mara ya nne, tangu uchaguzi wa vyama vingi uanzishwe nchini humo.

Safari ya Maalim Seif katika siasa za Tanzania ni ndefu, iliyojaa furaha na machungu, mafanikio na. Kabla ya kuwa miongoni mwa waasisi wa chama cha CUF Maalim Seif kwa muda mrefu alikuwa mwanachama wa chama tawala cha CCM, akipanda ngazi mbali mbali za kisiasa hadi kuwa waziri kiongozi wa Zanzibar chini ya utawala wa Rais Ali Hassan Mwinyi.

Baada ya kuhitimu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 1975, alitumika kama msaidizi wa rais wa zamani wa Zanzibar, Aboud Jumbe kutoka mwaka 1975 hadi 1977. Baadaye aliteuliwa kuwa Waziri wa Elimu, wadhifa aliotumika kwa miaka 3 hadi mwaka 1980.

Mwaka 1988, katika mageuzi ya mawaziri wakati wa awamu ya kwanza ya rais Idris Abdul Wakil, Maalim Seif aliondolewa kwenye wadhifa wa waziri kiongozi. Mwaka 1992 serikali ya Tanzania ilipobadilisha katiba na kuruhusu mfumo wa vyama vingi vya kisiasa, Seif Shariff na wenziwe ndipo walipochukuwa fursa hiyo na kuunda chama cha, CUF.

Maalim Seif alichukua fursa ya uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 kugombania urais wa visiwa vya Zanzibar na Pemba. Alishindwa na Dr. Salimn Amour wa CCM aliyepata asilimia 50.2 kwa asilimia 49.7 za Maalim Seif. CUF ililalamika kuwa matokeo hayo yalitokana na wizi wa kura na kuzusha ghasia za kisiasa. Maalim Seif aligombea katika chaguzi nyingine zilizofuata mwaka 2000 na 2005 dhidi ya Amani Abeid Karume wa CCM na zote ziliishia kwa mabishano makubwa wa matokeo huku CCM ikitangazwa mshindi na CUF ikidai kuibiwa ushindi.

Uchaguzi wa mwaka huu unafanyika katika mazingira hayo, ambayo yametia imani wananchi wa Zanzibar kuwa matokeo ya uchaguzi huu hayatazusha ghasia na mfarakano kama uliotokea katika chaguzi tatu zilizopita visiwani humo. Maalim Seif Shariff Hamad alizaliwa mtaa wa Nyali, Mtambwe kisiwani Pemba, mwaka 1943. Ana mke na watoto watano.

 

Dr. Wilbroad Peter Slaa: Mpinzani maarufu

Na Esther Githui-Ewart

Dr. Wilbroad Peter Slaa

Dr. Wilbroad Peter Slaa, mgombea urais kupitia tiketi ya chama cha CHADEMA ni miongoni mwa wanasiasa maarufu sana katika upande wa upinzani nchini Tanzania. Dr. Slaa mwenye umri wa miaka 60 alizaliwa Karatu, Arusha na kusomea upadre katika kanisa la Roman Katoliki ambako alipata shahada ya udhamirifu ya udaktari katika kanisa hilo.

Dr. Slaa anasifika kwa kujihusisha na maendeleo ya kijamii kwa miaka mingi , ikiwa ni pamoja na kuhudumu kama mkurugenzi wa shirika la maendeleo katika dayosisi ya Mbulu.

Mgombea Urais huyu ambaye amekuwa mbunge kwa miaka 15 ametoa mchango mkubwa wa maendeleo ya kijamii. Akiwa mbunge wa Karatu, alijishughulisha na usimamizi wa miradi ya maji na kuinua hali ya jamii alizoishi nazo.

Alichangia sana katika shirika linaloitwa ‘TWAWEZA’ kati ya mwaka wa 2005 hadi 2010 akiwa mbunge. Katika kura ya maoni iliyoendeshwa na kundi linaloitwa ‘Jamii Forum’, Dr. Slaa aliibuka kuwa mtu maarufu zaidi nchini Tanzania .

Katika upande wa sera Dr. Slaa anajinadi kwa kuahidi kupambana na ufisadi, kuunda uadilifu na kutoa kipaumbele kwa ubora wa elimu. Anaahidi usimamizi bora wa raslimali za Tanzania, kuhakikisha pato la haki linalotokana na raslimali za nchi na kutumia pato hilo kwa ujenzi wa taifa zima.

Lakini ni nini kinachomtenga yeye na wagombea wenzake wa kiti cha urais? Kwa mujibu wa mwenyekiti wa kamati ya kampeni zake Profesa Mwesiga Baregu watanzania wengi wanamuona kama mtu mwaminifu. Mtu muadilifu.

Uchaguzi Tanzania 2010

Uchaguzi Tanzania 2010

Maoni

Utamchagua nani kua rais wa Tanzania

Angalia matokeo »

Ibrahim Lipumba

Lipumba anadai tume ya uchaguzi ndio tatizo kubwa kwa upinzani

Lipumba anadai tume ya uchaguzi ndio tatizo kubwa kwa upinzani

Zaidi